Advertisements

Sunday, April 30, 2017

Milango ya kanisa yavunjwa Kibiti

By Mwandishi Wetu, Mwananchi mwananchipapers@mwananchi. co.tz

Baada ya kuwapo matukio ya mauaji walayani hapa, Kanisa Katoliki Kigango cha Jaribu/Mjawa katika Parokia ya Kibiti Mkoa wa Pwani, limevunjwa mlango wake na watu wasiojulikana kisha kuchoma moto majoho manne ya viongozi wa kanisa hilo.

Kiongozi wa kanisa hilo, Katekista Joseph Mwilu amesema tukio hilo limetokea juzi saa mbili usiku.

Mwilu amesema akiwa kwake alipigiwa simu na mweka hazina, Mastiga Elias anayeishi jirani na kanisa hilo kuwa kuna moto unaowaka kanisani hapo.

Amesema baada ya kupata taarifa hiyo amesubiri hadi asubuhi ya jana ndipo alipofika kanisani hapo na kukuta mlango umevunjwa.

Alifafanua kuwa baada ya kufika mlangoni aliona kuna karatasi iliyoachwa hapo kikiwa na maandishi yafuatayo.

“Tunatoa tahadhari, mmewaua ndugu zetu wawili siku ya Jumamosi, sisi leo tunaanza kazi, tuko 12 na hatushindwi. Kuanzia ngazi ya kijiji, kata hata wilaya, walimu, madaktari, manesi, watendaji wa vijiji na hata taasisi zote. Tunashukuru kwa ushirikiano wenu,” amenukuu kimemo hicho kilivyokuwa kimeandikwa.

Amesema baada ya kuingia ndani ya kanisa alibaini majoho manne ya viongozi wa kanisa hilo yalichomwa moto, mawili yakiwa yanayovaliwa na makateksta na mengine huvaliwa na watumishi wa misa.

Vilevile amesema alipoangalia kwa umakini mkubwa alibaini pia vitambaa vinne vya madhabahuni navyo vilikuwa vimechomwa moto na dirisha moja.

Kamanda wa Polisi mkoani Pwani, Onesmo Lyanga amethibitisha kwa njia ya meseji kutokea kwa tukio hilo.

“Tunafuatilia ili kupata taarifa kamili,” ulisomeka hivyo ujumbe huo.

No comments: