Advertisements

Saturday, June 24, 2017

SERIKALI YATOLEA UFAFANUZI KUHUSU ONGEZEKO LA IDADI YA WATU

                 Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb)

        Benny Mwaipaja, WFM, Dodoma
Serikali imeeleza kuwa pamoja na juhudi mbalimbali zinazofanywa na Serikali ikiwemo kutoa elimu juu ya uzazi wa mpango, suala la udhibiti wa ongezeko la idadi ya watu nchini ni mtambuka linalohitaji usimamizi na ushirikiano wa wadau wote.


Hayo yameelezwa Bungeni mjini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Kaliua Mhe. Magdalena Sakaya (CUF), aliyetaka kujua mpango wa Serikali wa kudhibiti ongezeko la watu hapa nchini ili liendane na uwezo wa Serikali wa kupeleka huduma muhimu kwa wananchi.

Dkt. Kijaji alisema kuwa, ongezeko la idadi ya watu nchini inatokana na vizazi au idadi kubwa ya watoto ambao akina mama wanazaa wakati wa uhai wao na ukosefu wa elimu kwa wasichana au akina mama.


“Tafiti zinaonyesha kuwa akina mama wenye elimu ya sekondari na kuendelea huzaa watoto wachache zaidi ikilinganishwa na wanawake wasiokua na elimu” alieleza Dkt. Kijaji

Dkt. Kijaji aliongeza kuwa, Tanzania ina Sera ya Idadi ya Watu iliyoridhiwa na Serikali mwaka 1992 lengo la sera hiyo ni kupunguza kasi ya ongezeko la idadi ya watu ili kuhakikisha kuwa, idadi yao inaendana na huduma za jamii zilizopo. 

“Mambo yaliyobainishwa katika sera hiyo ni namna Serikali ilivyojipanga kutoa elimu ya msingi na sekondari, usawa kijinsia, umri wa kuolewa, matumizi ya njia za kisasa za uzazi na wajibu wa kila mdau tukiwemo sisi Waheshimiwa Wabunge”. Alisema Dkt. Kijaji.


Aidha, alisema kuwa utafiti wa Afya ya Mama na Mtoto ya mwaka 2015/2016 umeonesha kuwa endapo mtoto wa kike atakaa shuleni kwa kipindi kirefu, uwezekano wa kuzaa watoto wengi ni mdogo kwa vile elimu inamsaidia kujitambua na inampa uwezekano mkubwa wa kujishughulisha na shughuli nyingine za kiuchumi na matumizi ya njia bora ya uzazi wa mpango. 


Katika swali la nyongeza Mbunge wa Kaliua Mhe. Magdalena Sakaya, alihoji pamoja na kuwepo sera ya kudhibiti ongezeko la watu nchini, bado katika maeneo ya vijijini watu wanazaa watoto wengi hali inayo sababisha watoto kuishi katika mazingira magumu na kukosa huduma za msingi na kuhoji endapo Serikali ipo tayari kutangaza ukomo wa watoto katika familia.

Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Kijaji, amesema kuwa Serikali haiwezi kuweka ukomo wa idadi ya watoto katika familia kwa sababu linahusisha masuala ya mila, desturi na tamaduni za Taifa.

No comments: