Advertisements

Monday, October 23, 2017

NASA yatangaza maandamano ya siku mbili


Kiongozi wa Muungano wa National Super Alliance (Nasa), Raila Odinga ametangaza maandamano ya siku mbili kuanzia kesho.
Odinga akizungumza katika Kanisa Katoliki la St Peter’s Kiminini, Trans-Nzoia amesema maandamano ya kesho Jumanne Oktoba 24,2017 na Jumatano yanalenga kushinikiza Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kufanya mageuzi kabla ya kuandaa uchaguzi wa urais wa marudio.
“Jumanne kutakuwa na maandamano, Jumatano pia tutaandamana na Alhamisi hakuna uchaguzi,” alisema Odinga ambaye amesusia uchaguzi huo wa marudio wa Oktoba 26,2017.
Wiki iliyopita Odinga alisema angetoa mwelekeo halisi Oktoba 25,2017 kuhusu hatua ambayo wafuasi wake watachukua wakati wa uchaguzi huo.
Kiongozi huyo wa upinzani amesema maandamano ni haki ya kikatiba ya Wakenya hivyo waandamanaji hawapaswi kuadhibiwa kwa kupigwa risasi na polisi.
Raila amedai ana ushahidi wa kuonyesha kuwa uchaguzi wa Oktoba 26 umesheheni udanganyifu.
“Tuna ushahidi wa kuonyesha kuwa uchaguzi wa Alhamisi una dosari. Tayari magari ya polisi yanasafirisha karatasi za kura. Ukweli ni kwamba kiasi kikubwa cha kura zilichapishwa jijini Nairobi na wala si Dubai kama mnavyoelezwa,” alisema.
Alidai kuwa kujumuishwa kwa Cyrus Jirongo katika karatasi za kura ni ithibati kwamba karatasi za kura zilichapishwa nchini Kenya.
“ Jirongo alitangazwa na korti kuwa amefilisika, mbona IEBC ilimjumuisha katika karatasi ya kura? Walijumuisha wagombea wote wanane kwa sababu karatasi zilikuwa zimechapishwa na Jubilee jijini Nairobi,” alisisitiza Odinga.
Alisisitiza kuwa hatashiriki uchaguzi wa Alhamisi ambao utawahusisha Rais Uhuru Kenyatta, Mohamed Abduba Dida, Dk Ekuru Aukot, Cyrus Jirongo, Dk Japhet Kaluyu, Profesa Michael Wainaina na Joseph Nyagah.
“Uhuru hana mshindani, anashindana peke yake. Sisi tunahitaji uchaguzi ambao Uhuru anashindana na Raila bali si uchaguzi wa mtu mmoja,” alisema.

Chanzo: Mwananchi

No comments: